KIMATAIFA KITAIFA

MKURUGENZI WA FAO AIPONGEZA TANZANIA UTEKELEZA MPANGO WA BBT

MKURUGENZI WA FAO AIPONGEZA TANZANIA UTEKELEZA MPANGO WA BBT

MKURUGENZI MKUU wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) Dkt. Qu Dongyu amesema kuwa Shirika hilo limevutiwa na mradi wa kuwawezesha vijana unaotekelezwa na Serikali ya Tanzania wa Jenga Kesho Iliyobora “Building Better Tomorrow” (BBT).

“FAO tutaunga mkono mradi huu ili Serikali ya Tanzania iweze kutimiza malengo ya kuwainua vijana na wanawake kwenye sekta ya kilimo kama ilivyo moja ya agenda kwenye mkutano wa FAO wa mwaka 2023”.

Ameyasema hayo jana (Jumatano, Oktoba 18, 2023) alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa katika ofisi za Makao Makuu ya FAO zilizopo Rome, Italia. Waziri Mkuu yuko nchini Italia akimuwakilisha Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika Mkutano wa Jukwaa la Kimataifa la Chakula Duniani ulioanza Oktoba 16 hadi Oktoba 20, 2023.

Aidha, Mkurugenzi huyo amempongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendeleza sekta ya kilimo pamoja na kuboresha mahusiano na mashiriki ya kimataifa.

Dkt. Dongyu ameahidi kutembelea Tanzania mwaka 2024 kwa ajili ya kujionea maendeleo katika sekta ya kilimo pamoja na kupanua wigo wa majadiliano kati ya Tanzania na Shirika hilo ili kuendelea kuwezesha zaidi sekta ya kilimo na uchumi wa Buluu.

Kwa upande wake, Waziri Mkuu alisema kwa sasa Serikali ya Tanzania inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan imeanza kupanua wigo wa kilimo kutoka cha kutegemea mvua na kujikita zaidi kwenye kilimo cha umwagiliaji, ambapo imetenga shilingi bilioni 900.

About Author

Bongo News

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *