KITAIFA

RAIS SAMIA AKUNWA NA UTENDAJI WA WAZIRI ULEGA

RAIS SAMIA AKUNWA NA UTENDAJI WA WAZIRI ULEGA

Rais wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameipongeza Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kusimamia ipasavyo mpango wa Serikali wa Kuijenga kesho bora kupitia Kilimo (BBT) hasa kwa vijana ambao umeonyesha mafanikio kwa asilimia kubwa.

Rais Dkt. Samia amesema hayo leo Agosti 08, 2023 wakati akikagua mabanda mbalimbali kwenye maonyesho ya Wakulima nanenane 2023 jijini Mbeya akiwa kwenye moja ya banda la mifugo linalosimamiwa na binti ambaye alianzisha mradi wa ufugaji muda mfupi baada ya kuhitimu masomo yake.

Mhe.Dkt. Rais Samia ameeleza kufurahishwa na namna vijana walivyojiajiri kwenye maeneo ya Mifugo na Uvuvi kupitia wataalam badala ya kusubiri ajira pekee na kuridhishwa pia na Wizara hiyo inavyosimamia kuhakikisha vijana wanajiajiri kupitia Kilimo kama ufugaji na uvuvi.

“Lakini nataka niseme wataalamu, kutoka mwaka jana (2022) mpaka sasa hivi (2023) kwa upande wa Mifugo na Uvuvi maendeleo ni makubwa. Mnakumbuka mwaka jana tuligombana uwanjani pale nikasema hamjafanya chochote na mmeona nilichokifanya, nilipompandisha huyu bwana (Waziri wa Mifugo) nikamwambia nakupa miezi sita nione ulichokifanya usipofanya nawewe utaondoka kama alivyoondoka mwenzio sasa leo ninashukuru na najua sio yeye ni ninyi wataalamu”, Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan akizungumza kwenye moja ya banda la mfugaji ndani ya Uwanja wa John Mwakangale jijini Mbeya.

Pamoja na kueleza mengi, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdalah Ulega amesema Wizara ina matamanio ya kuona mifugo hasa ng’ombe wanaonenepeshwa na wajasiriamali mbalimbali nchini wanauzwa kwa faida ndani na nje ya nchi na kwa kutumia mitandao ya kijamii.

“Mhe.Rais (Samia S. Hassan) hawa Ng’ombe watakuwa wakipigwa picha hatua kwa hatua katika bapa la uso na mwili mzima anapoingia toka anaponunuliwa lengo letu kwasababu hawa (wafugaji) ni wafanyabiashara tunawapa platform ya Digital (fursa ya utandawazi) kama BBT ilivyo malengo yake. Lengo letu ni kwamba wawe na uwezo hata wa kuuza katika mitandao na hivi sasa tunaishukuru Wizara ya fedha imetukubalia na ina mpango maalumu wa kutuingiza katika masoko ya kimtandao”, Mhe. Abdalah Ulega, Waziri wa Mifugo na Uvuvi.

Pia Waziri Ulega ametumia fursa hiyo kuziomba taasisi za kifedha (Benki) kuendelea kutoa ushirikiano kwenye kuwezesha unenepeshaji wa Ng’ombe ili kuendelea kuwaunga mkono wafugaji.

Hata hivyo amewataka wananchi hususani vijana kote nchini kuendelea kuchangamkia fursa za Kilimo cha aina mbalimbali hasa mifugo na uvuvi ili kuendesha maisha yao.

About Author

Bongo News

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *